Tuesday, August 13, 2013

Mambo ya sirini aliyonayo mwanadamu.


Shalom! Shalom!

Watashindanaaa! Lakini hawatashinda.

Hizi ni baadhi tu ya salamu tunazoweza salimiana sisi tumwaminio Kristo Yesu, na tuliyo katika madhabahu ya Bwana inayoongozwa na Mchungaji, Antony Lusekelo (supa chaji).

Nikukaribishe basi katika safu hii, ambapo kama kawaida unapata nafasi ya kujua kile kilichojiri katika madhabahu ya Ubungo, Kibangu katika siku zote za Ibada.

Ndani ya juma hili ambalo lilikuwa na wingi wa sherehe za kitaifa kwa maana ya nane nane, pamoja na sherehe ile ya kidini ya ndugu zetu Waislamu (Eid Mubarak), Mchungaji Antony Lusekelo alikuwa na mfululizo wa somo alilolipa jina la Mambo ya sirini, aliyonayo mwanadamu.

Somo hili lilianza rasmi katika siku ya Alhamisi, huku Mchungaji akiviweka bayana vitu hivyo vya sirini alivyonavyo binadamu, kuwa ni roho, malaika, pamoja na nyota, ambapo kwasasa alizama katika elimu ya nyota.

Ni wazi kuwa kwa kipindi sasa Wakristo tumeyatupilia mbali masomo ya nyota, tukiamini kuwa huwenda imani hiyo iko nje ya imani tuliyonayo, suala ambalo Mchungaji anaweka wazi kuwa si sahihi.

Katika ibada ya juzi, yaani ya Jumapili ya tarehe 11 mwezi agosti, Katapila aliamua kuutoa utata huo kwa kusema kuwa, kila binadamu anayo nyota yake, nyota ambayo inamtofautisha na mtu mwingine yeyote.

Aidha Mchungaji alitoa mfano wa Yusufu alipokuwa akiwaelezea familia yake juu ya ndoto yake, aliyoota nyota zikimwatamia pamoja na mfano wa Mamajusi wa Mashariki, waliyoiona nyota ya Kifalme ya Kristo Yesu Mnazareti, kama udhihirisho tu wa kuwa kila mtu anayo nyota yake.

Katika kudadavua zaidi somo hili la nyota kupitia Biblia, huku akiweka wazi kuwa nyota yaweza kufishwa au kung’azwa, Katapila alisoma neno;

Neno: Ufununo wa Yohana 2:26-28. 

26Na yeye ashindaye, na kuyatunza matendo yangu hata mwisho, nitampa mamlaka juu ya mataifa.27naye atawachunga kwa fimbo ya chuma, kama vyombo vya mfinyanzi vipondwavyo, kama mimi nami nilivyopokea kwa Baba yangu.28Nami nitampa ile nyota ya asubuhi.

Mchungaji alisema kuwa nyota ya mtu ndiyo inayoweza kumsababishia kibali kwa watu, baraka, mafanikio, na hata  maendeleo. Ila endapo nyota hiyo itafishwa, ndipo ambapo mikosi, laana, ajali, kudidimia kimaisha  na mambo mengine mabaya kama hayo, humpata mtu.

“mtaa unaokaa, pamoja na watu unaokaa nao wanaweza kufisha nyota yako,  na ndiyo maana nitakuombea asubuhi ya leo juu ya nyota hiyo, Mungu airudishe na ing’ae” aliongeza Mchungaji.

Mengi aliyasema King Kong katika suala hili la nyota, lakini haswahaswa alikuwa akisisitiza kuwa, inampasa kila mtu kumwomba Mungu juu ya nyota yake, kwani ni moja kati ya vitu vya muhimu katika maisha ya mwanadamu.

Hata hivyo Mchungaji hakuishi hapo, kwani aliwaonya watu juu ya uadui na kusema kuwa, si vyema mtu akatengeneza maadui huku akikataza pia watu kuuwana pasipo sababu.

Dokezo.
(Haya ni baadhi tu ya maneno aliyoyasema, na kuyahubiri Mchungaji Lusekelo Antony, akisindikizia somo la siku).

“ukija kanisani, shiriki kila jambo, na acha kudandia treni kwa mbele”.

“mimi ni Mchungaji niliyosomea sana wito wangu, na nina uzoefu wa miaka zaidi ya 30”.

“elimu ni zaidi ya kukaa darasani,. Elimu ni uwezo wa kuyatawala mazingira yako”.

“kama wewe ni kijana, soma sana katika fani yako, kwani Biblia imesema Mshike sana elimu, usimuache aende zake”.

“wamebarikiwa sana wanaomjua bwana Mungu wao. Mjue sana Mungu, ndipo mema yatakavyo kuijilia”.

“ibada hizi zinakusogeza karibu na Mungu. Pia itakurudishia kiu ya kwenda, kanisani”.

“upandacho, ndicho utakachovuna. Usimtende ubaya mtu anayekuamini”
“usishindane na asiyekudhuru, wala kupanga kumpiga mwenzako, kwa siri ni mwiko”.

“unapompa mtu nafasi ya kukujua, unampa shetani nafasi. Mfano ni Samsoni, alimpa nafasi Delila ya kumjua”.

“mwanamke au mwanaume, anapokuja au mnapokutana na rafiki wa mumeo au mkeo, acha kuchangamka sana, mkaribishe kisha kaa mbali waache waongee kama wanaume kwa wanaume, au wanawake kwa wanawake na si kuyatawala maongezi yao”.

“mwiko kuitawala nyumbaya mwanaume mwenzio, wala kumuita mwanaume mwenzio bwana mdogo mbele ya mkewe, hata kama umemzidi umri”.

“Muheshimu mtu kwa wajibu wake”.

“Ukimkuta kijana anaumri wa miaka arobaini na ana nyumba 3, halafu wewe huna japo umemzidi umri, ni Mzee kwako, muheshimu na umpe shikamoo!”

Kwa mengi au kwa machache, hayo ndiyo yaliyojiri Jumapili ya jana madhabahuni kwa bwana GRC, Ubungo Kibangu kwa Mchungaji Lusekelo Antony maarufu kama Katapila, au Mzee wa Upako.

Uwe na wiki njema. 

Barikiwa!



0 comments:

Post a Comment