Watashindanaaaaa!
Natumai umzima na upo tayari kujua kile ambacho
kilijiri madhabahuni mwa bwana, Ubungo Kibangu kwa Mzee wa Upako, jana Alhamisi
ya tarehe 1/8/2013.
Kwa wale wenzangu na mie tuliyoweza kufika
madhabahuni hapo, naamini kabisa tulipata kitu cha tofauti ndani ya mioyo yetu,
tangu pale tulipoanza kwa kumsifu Mungu na kumwabudu (Praise & Worship),
mpaka alipoingia baba yetu wa kiroho, Mchungaji Antony Lusekelo.
Kama kawaida tuliabudu kwa pamoja na baada ya hapo,
Mzee wa Upako aliongoza sala iliyojaa utulivu wa roho mtakatifu, huku akimwomba
Mungu atuonekanie tangu kwenye ibada ile, hata katika maisha yetu kwa ujumla.
Baada ya maombi hayo, tulimsifu Mungu huku
tukiongozwa na yeye (Mchungaji), kwa pambio la ‘Yesu namba moja’ ambapo kwa hakika tulilitukuza jina la Bwana Yesu
kwa furaha kuu, na kisha tukaingia katika neno.
Ujumbe:
OMBA PASIPO KUKATA TAMAA.
Neno;
Luka 18:1 “Akawaambia mfano, ya kwamba imewapasa kumwomba Mungu sikuzote, wala
wasikate tamaa.
Hili ndilo somo, pamoja na neno lililotumika hiyo
jana, yaani Alhamisi ya tarehe mosi, mwezi wa nane.
Mchungaji alianza kulielezea neno hili, kwa kutoa
mfano kuwa wapo watu wengi ambao hulalamika sana kwamba, wameombewa katika
makanisa mengi pasipo mafanikio, na kusema kuwa wengi wao hukata tamaa njiani
huku wengine wakitaka kumtumia Mungu kama njia tu ya kutokea, na si kwamba
wanampenda na kumuhitaji.
“Mara nyingi tunashindwa kufanikiwa, kwasababu
hatumtaki Mungu, tunataka nguvu zake tu” alisema Katapila na kuongeza kuwa, kwa
mtindo huo kamwe hatuwezi kumwona Yawe.
Katika kusisitiza hilo, Mchungaji alisema kuwa inampasa
kila mtu kumwamini Mungu na kumpenda, na si kuishia kuzipenda kazi zake tu, kwa
mfano wa baadhi ya watu waliyomfuata Yesu kwasababu ya mikate.
Vilevile Mchungaji aliwekawazi kwamba katika maombi
yoyote yale, ni lazima msingi mkuu wa maombi hayo uwe ni bidii pamoja na imani,
itakayokufanya wewe usikate tamaa.
Kukata tamaa ni jambo ambalo Mchungaji alilikemea
kwa nguvu na mifano mbalimbali, kama ule wa Mitume kumi na wawili ambapo baada
ya kupaa kwa Yesu, wanafunzi hao walipitia magumu mengi ikiwemo kuuawa kwa
Yakobo (mwanafunzi wa Yesu).
“Jambo hili la kuuawa kwa Yakobo halikuwakatisha
tamaa wanafunzi wa Yesu, wala halikuwafanya wakufuru, zaidi tu walizidi
kusongambele na hatimaye wakaweza kuijenga misingi imara ya Kanisa” alisema
Transformer.
Ni wazi kuwa mtumishi huyu wa Mungu, alikuwa
akijenga roho ya kumtumaini bwana mioyoni mwetu,pamoja na roho ya bidii katika
kumlilia Mungu kwenye mahitaji yetu, vitu ambavyo tunaweza kuvitumia kama
nyenzo ya kufika kule tuendako.
Lakini kutokana na ukaribu aliyonao Mchungaji
Lusekelo kwa Mungu, na katika kuzidi kufafanua zaidi juu ya maombi, yeye aliweka
wazi jambo fulani na kusema kuwa, ”Ukiombewa na mimi halafu usifanikiwe, nenda uendako
hutofanikiwa wala kupona milele, kwasababu najua Mungu anavyonisikia”.
Kauli hii inaonyesha wazi kuwa, kumbe nae mtumishi
huyu wa Mungu huomba kwa bidii, na kwa dhati kiasi cha kuamini kuwa kama hitaji
lako lisipoisha ukiwa katika madhabahu ile ya Ubungo Kibangu, basi hitaji hilo
halitoweza kuisha mahali popote pale, chini ya jua.
Ni wazi kuwa maombi yana nguvu na huwatoa watu
katika vifungo mbalimbali vya magonjwa, laana, mikosi, umasikini na kila hila
za Yule muovu shetani na ndiyo maana Mchungaji Antony Lusekelo, kwa siku ya
Alhamisi ya jana, aliamua kusisitizia suala la kuomba pasipo kuchoka wala
kukata tamaa, mpaka pale Mungu atakapo jibu mahitaji yetu.
Kwa kifupi hayo ndiyo yaliyojiri jana katika
madhabahu ya Ubungo Kibangu, kwa Mzee wa Upako.
Karibu nawe Jumapili ya tarehe 4/8/2013, tuabudu
pamoja na kujifunza mengi juu ya Ufalme wa Mungu aliyetuumba.
Jinsi
ya kufika; Panda gari la Ubungo, shuka Riverside
kituo ambacho kipo karibu na LandMark Hoteli, hapo utaona bango la Mtumishi wa
Mungu Antony Lusekelo, linaloelekeza njia ya kuelekea kanisani. Waweza panda
pikipiki, taxi au mabasi ya kanisa yanayosafirisha waumini, BURE!
Kwa
mawasiliano ya ujumbe mfupi wa maandishi (sms); +255(0)713
725 473.
Watashindana, lakini hawatashinda!
Tutapanga mipango, itapangika!
Wakituloga, imekula kwao!
Kwetu, hakuna kudumaa!






0 comments:
Post a Comment